RAIS John Magufuli ametakiwa kutumbua jipu kwa baadhi ya watendaji wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam wanaoingia mikataba bila kufuata sheria na kanuni, anaandika Regina Mkonde.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mwita Waitara, Mbunge wa Jimbo la Ukonga na Mwenyekiti wa wabunge wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) Mkoa wa Dar es Salaam wakati akiwa katika Ofisi za Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam.
Waitara amedai kuwa, kuchelewa kupatikana kwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam kunatumiwa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuingia mikataba mikubwa kinyume cha sheria bila kuwa na meya.
“Haiwezekani mikataba ya miradi mikubwa kama wa mabasi ya mwendo kasi DART kushughulikiwa na watu watano bila ya kusubiri kupata baraka kutoka kwa Meya wa Jiji,” amesema Waitara.
Waitara amesema kuwa, mbinu zinazotumika kuvuruga uchaguzi huo ni kukamilisha utekelezaji wa mikataba yote mikubwa kabla ya Ukawa kushikilia jiji na kuvumbua makosa yaliyopo katika mikataba hiyo.
Amesema, kitendo cha Rais Magufuli kukaa kimya kinatafsri kuwa na nia ya kuharakisha mikataba hiyo ya jiji kukamilishwa kabla kumilikiwa na Ukawa ili kuficha makosa yao na kuyaelekeza kwa Ukawa.
“Kwa sababu yeye alikuwa Waziri wa Ujenzi katika serikali iliyoipita anaogopa kutumbuliwa jipu la mradi wa DART, ndiyo maana hataki kuharakisha uchaguzi wa Meya kufanyika,” amesema.
No comments:
Post a Comment